Monday 4 August 2014

Daktari aambukizwa Ebola nchini Nigeria

Daktari aliyemtibu mgonjwa wa Ebola ameabukizwa nchini Nigeria
Daktari mmoja jijini Lagos Nigeria aliyemtibu mgonjwa aliyefariki kutokana na homa ya Ebola amepatikana ameambukizwa na maradhi hayo.

Daktari huyo ambaye alimtibu mfanyikazi wa wizara ya hazina nchini Liberia aliyepatikana na homa hiyo ya Ebola na kuwa mtu wa kwanza kuaga dunia nchini Nigeria sasa amedhibitishwa kuambukizwa .
Waziri wa afya nchini humo Onyebuchi Chukwu amesema kuwa daktari huyo pamoja na watu wengine 70 waliokutana na marehemu wametengwa kwa uchunguzi na matibabu zaidi.
Mataifa yaliyoathirika na homa ya Ebola
Patrick Sawyer alitua nchini Nigeria Julai tarehe 20 na akafa tarehe 25 katika hospitali moja mjini Lagos.
Mlipuko huu wa ugonjwa wa ebola katika ukanda wa magharibi mwa Afrika umesababisha vifo vya watu zaidi ya 826 katika mataifa ya Guinea, Liberia na Sierra Leone.