Monday 25 August 2014

Waziri Kawambwa aiasa Jamii Kuchangia Elimu

Aipongeza Airtel kwa kutoa vitabu

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dkt. Shukuru Kawambwa ameiasa jamii kuchangia kuboresha elimu nchini kwa kutoa misaada mbalimbali itakayosaidia kuimarisha ubora wa elimu inayotolewa katika ngazi mbalimbali za elimu.

Waziri Kawambwa alikuwa akizungumza katika hafla  ya uzinduzi wa Mradi wa Vitabu Airtel Shule Yetu 2014 jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki ambapo wawakilishi wa shule  za Sekondari 30 walipatiwa msaada wa vitabu vya Sayansi na Hisabati na Kampuni hiyo.





Waziri Kawambwa ambaye alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo alisema Mradi huu wa Vitabu Airtel Shule Yetu utakuwa wa manufaa makubwa sana si kwa  wanafunzi shuleni tu bali kwa sekta nzima ya Elimu hapa nchini na kwa Taifa kwa ujumla.  

Sote tunatambua kwamba kitu pekee kinachotofautisha nchi zilizoendelea na zinazoendelea siyo utajiri na mali walizonazo bali ni elimu na ujuzi.  Hii ni kwa sababu utajiri na mali havijileti vyenyewe isipokuwa huchochewa na maendeleo mazuri yaliyo jengwa katika msingi mzuri wa ELIMU. Kwa kadri kiwango cha elimu na ujuzi au maarifa kinapokuwa juu katika nchi, ndipo na kiwango cha maendeleo ya nchi yanapozidi kukua katika nchi hiyo,”alisema Dkt. Kawambwa.

Dhamira ya Dira ya Maendeleo ya Mwaka 2025 (Tanzania Development Vision 2025) ni kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.  Lakini hilo litawezekana tu kwa kupitia elimu.  Yaani kuwa na Taifa lililoelimika; lenye wasomi wanaoweza kubaini na kutatua matatizo ya maendeleo ya nchi yetu.  Na katika wakati huu tulionao, Sayansi na  Tekinolojia vina nafasi  ya  pekee katika maendeleo ya nchi na ustawi wa jamii. 

“Tunaishukuru sana Airtel Tanzania kwa kutuunga mkono katika dhamira ya Serikali yetu ya kuwekeza katika sekta ya elimu nchini.  Airtel imekuwa mstari wa mbele katika kuchangia vitabu pamoja na misaada mbalimbali kwa shule zetu hapa nchini.  Vitabu hivi vilivyochangiwa na Airtel vitasaidia sana katika juhudi za Serikali za kuimarisha ubora wa elimu inayotolewa,” alisema Waziri Kawambwa. 


Hivi sasa kuna uhaba wa walimu wa masomo ya Sayansi na Hisabati katika shule zetu za Sekondari hapa nchini.  Takwimu zinaonesha kwamba hadi mwaka 2013/14 tulikuwa na upungufu wa walimu wa Sayansi na Hisabati 26,998.  Lakini hata kule kwenye walimu wa masomo haya bado kuna tatizo la uhaba wa vitabu.  Lakini kule ambako kuna uhaba wa walimu uwepo wa vitabu hivi utakuwa ni wa msaada sana kwa wanafunzi kuweza hata kujisomea wenyewe.  

Tukio hilo la Kampuni ya Airtel kukabidhi vitabu ni mwendelezo wa mambo mengi ambayo yamekwishafanya katika kuisadia Sekta ya elimu nchini.  Mradi huu ulianza miaka takriban kumi iliyopita na katika kipindi chote hiki mradi umeweza kupeleka vitabu na vifaa vya maabara katika shule mbalimbali na pia kufanya ujenzi na matengenezo katika shule kadhaa hapa nchini.  

Napenda kutumia fursa hii kuwahimiza makampuni mengine  na Taasisi mbalimbali nchini kuiga mfano huu wa Airtel na kusaidia sekta ya elimu ili kujenga taifa lililo bora.  Serikali iko tayari kushirikiana na Taasisi, Makampuni na asasi mbalimbali katika kuendeleza Elimu ya watoto na vijana wetu,” alisema Waziri Kawambwa. 

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Airtel Tanzania Sunil Colaso alisema kampuni yake itaendelea kuisaidia sekta ya elimu ili kuchangia katika juhudi za serikali za kuboresha elimu hapa nchini ambapo hadi hivi sasa shule za sekondari 1,000 zimefaidika kwa kupewa vitabu na kampuni hiyo.